Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA

ISO 9001:2015 Imethibitishwa Kutoa Huduma za Hali ya Hewa kwenye Usafiri wa Anga

Seasional Forecast

MWELEKEO WA MVUA ZA MSIMU WA MASIKA MACHI – MEI, 2026

Dondoo muhimu za msimu wa mvua za Masika (Machi – Mei), 2026

Taarifa hii inatoa uchambuzi wa mwenendo wa mifumo ya hali ya hewa na mwelekeo wa mvua za Masika kwa maeneo yanayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka (kanda ya Ziwa Victoria, nyanda za juu kaskazini mashariki, pwani ya kaskazini pamoja na maeneo yaliyopo kaskazini mwa mkoa wa Kigoma) katika kipindi cha miezi ya Machi hadi Mei, 2026. Ushauri na tahadhari umetolewa kwa wadau wa sekta mbalimbali wanaotumia taarifa za hali ya hewa katika utekelezaji wa majukumu yao kama vile kilimo na usalama wa chakula, mifugo na uvuvi, maliasili, wanyamapori na utalii, nishati na madini, maji, ujenzi, usafiri na usafirishaji (nchi kavu, kwenye maji na angani), mamlaka za miji, afya, sekta binafsi pamoja na menejimenti za maafa. Muhtasari wa mwelekeo wa mvua hizo na athari zake ni kama ifuatavyo:

a) Mwelekeo wa mvua za Masika kwa maeneo yanayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka:

  1. Mvua za Wastani hadi Juu ya Wastani zinatarajiwa katika maeneo mengi ya pwani ya kaskazini pamoja na baadhi ya maeneo ya magharibi mwa ukanda wa Ziwa Viktoria (mikoa ya Kagera na Geita) pamoja na kaskazini mwa mkoa wa Kigoma. Aidha, mvua za Wastani hadi Chini ya Wastani zinatarajiwa katika maeneo ya nyanda za juu kaskazini mashariki na baadhi ya maeneo ya ukanda wa Ziwa Viktoria (mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Mara na Simiyu).
  2. Mvua za Masika zinatarajiwa kuanza wiki ya nne ya mwezi Februari na ya kwanza ya mwezi Machi , 2026 katika maeneo ya kanda ya Ziwa Victoria; na wiki ya kwanza na ya pili ya mwezi Machi katika maeneo ya pwani ya kaskazini; na wiki ya pili na ya tatu ya mwezi Machi, 2026 katika maeneo ya nyanda za juu kaskazini mashariki. Mvua zinatarajiwa kuisha wiki ya nne ya mwezi Mei na wiki ya kwanza ya mwezi Juni 2026 katika maeneo mengi yanayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka.
  3. Ongezeko la mvua linatarajiwa mwezi Aprili, 2026.

b) Athari zinazotarajiwa:

  1. Vipindi vya unyevu wa kuzidi kiasi pamoja na mafuriko vinaweza kujitokeza na kuathiri ukuaji wa mazao katika baadhi ya maeneo, hususan yanayotarajiwa kupata mvua za Wastani hadi Juu ya Wastani.
  2. Kina cha maji katika mito, mabwawa na hifadhi ya maji ardhini kinatarajiwa kupungua hususan katika maeneo yanayotarajiwa kupata mvua za Wastani hadi Chini ya Wastani.
  3. Magonjwa ya mlipuko yanaweza kujitokeza kutokana na uchafuzi wa maji.

Kwa taarifa zaidi tafadhali pakua